Katika kukabiliana na hali yamaisha, siku hadi siku binadamu ameendelea kubuni na kuibua teknolojia mpya ili kupambana na hali ya maisha na mabadiliko ya tabia nchi na kuongeza uzalishaji kwa lengo la kujipatia kipato zaidi.
Wataalamu wa kilimo wamegundua
uwezo mkubwa wa mmea wa Azolla wenye utajiri wa virutubisho kwa ajili ya kulisha
mifugo aina zote mmea ambao unawezekana kupatikana kwa kuuotesha katika eneo
dogo ambalo kila mfugaji anaweza kumudu kuuzalisha.
Afisa Mifugo Halmshauri
ya Arusha Sakina Galle anazungumzia mmea
wa Azolla kuwa ni mmea wa asili kutoka jamii ya
‘Fern plant’ ambao asili yake ni nchini Australia japo kuwa mmea huu kwa
sasa umeenea na kuwa maarufu katika nchi za bara la Asia kama China, India hata
Afrika.
Katika bara la Afrika
Azolla inapatikana katika aina tisa ambazo kati ya hizo aina mbili za mmea wa
Azolla zimeshafanyiwa majaribio ambazo kwa kitaalamu ni Azolla Pinnata na
Azolla Ficiculoides na zote zinafaa kwa kulishia mifugo.
Galle ameendelea
kueleza kuwa mpaka sasa mmea huu umeanza
kuoteshwa nchini Tanzania na kuthibitisha kuwa mmea wa Azolla umeweza kustawi
muda mfupi baada ya kuoteshwa na kuonesha mafanikio ya haraka kwa wafugaji.
Licha ya kuwa mmea wa
Azolla kuthibitika kuwa na virutubisho bora kwa mifugo Galle amevitaja virutubisho kuwa ni pamoja na aina
nyingi za vitamini, protini, tindikali ya amino na madini muhimu yanayohitajika
kwa wanyama na kufanya mmea huo kuwa bora kwa kulishia wanyama wafugwao.
Aidha Galle amesema kuwa
virutubisho vinavyopatikana kwenye mmea wa Azolla unatumika mifugo mbalimbali
ikiwemo kuku, ng’ombe, mbuzi, kondoo, sungura, nguruwe na samaki.
Galle pia ameeleza
namna ya kuotesha mmea wa Azolla na kusema kuwa mmea wa Azolla unaoteshwa kwenye maji yaliyosimama
kwa maana ya kutengeneza bwawa lenye maji kasha kuweka mchanganyiko wa mbegu za
Azolla, dawa maalumu ya kupandia, udongo,
mchanga na mbolea ya samadi.
Kwa mara ya kwanza
uvunaji wa Azolla unafanyika siku 15 baada ya kuoteshwa na baadae uvunaji
hufanyika kila baada ya siku mbili
mpaka tatu na kuendelea kuvuna kwa muda wote.
Aidha mmea wa Azolla
unamsaidia mfugaji kupunguza gharama za chakula kwa asilimia hamsini mpaka mia (50%
- 100%) kwa kuchanganya mmea huo na vyakula vingine vya mifugo na wakati
mwungine mfugaji anaweza kulisha mmea huo peke yake.
“Virutubisho vya mmea
wa Azolla husaidia kupunguza magonjwa kwa mifugo na kuongeza uzito kwa haraka
na kwa wanyama kama kuku husaidia kuongeza utagaji wa mayai” amesema Galle.
Aidha Galle amewataka wafugaji kujifunza kuzalisha na kutumia
mmea wa Azolla kulishia mifugo yao kwani upatikanaji wake na rahisi na wa
gharama nafuu.
No comments:
Write comments